Rwanda yajitetea kuhusu ushuru
Kwa ufupi
Ni ule wa kupandisha tozo za magari iliyopandishwa na nchi hiyo kwa madai ya kufanya ulinganifu
Dar es Salaam/Dodoma. Wakati ushuru wa magari
makubwa ukiwa umeshushwa kwa wiki moja, Serikali ya Rwanda imejitetea
ikisema haijafanya hujuma yoyote dhidi ya Tanzania, bali imepandisha
tozo hiyo ili kuifanya ilingane na ile inayolipwa Tanzania.
endelea.......
endelea.......
Akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake jana,
Balozi wa Rwanda nchini, Ben Rugangazi alisema kuongezwa kwa ushuru huo
wa forodha kisichukuliwe kama jaribio la kutaka kuvuruga uhusiano kati
ya nchi hizi mbili.
Balozi Rugangazi alisema Rwanda imeamua kupandisha
kiwango chake kutoka Dola za Marekani 152 (Sh240,000) kuwa Dola 500
(Sh790,000) ambazo pia hutozwa na Serikali ya Tanzania kwa muda mrefu.
“Kumekuwa na majadiliano ya muda mrefu ili kuleta
ulinganifu wa ushuru wa forodha kwani kwa muda mrefu wafanyabiashara
Rwanda wamekuwa wakilalamika kutokana na kushindwa kushindana vizuri
kwenye soko la biashara kutokana na tofauti kubwa ya ushuru wa forodha.
“Hili suala tulishawahi kuliwasilisha katika
Jumuiya ya Afrika Mashariki tukawaomba wasaidie kurekebisha kasoro hiyo,
lakini hawakufanya hivyo. Sasa tumeamua kuchukua hatua hii ili kwenda
sambamba na wenzetu Tanzania.
“Pande zote Tanzania na Rwanda zilikubaliana kuwa
ushuru mpya ungeanza kutumika Septemba mwaka huu na ndivyo ilivyokuwa,”
alisema Balozi Rugangazi.
Siku saba
Kutokana na msongamano wa malori kwenye mpaka wa nchi hizo mbili, Serikali ya Rwanda imeshusha ushuru kwa wiki moja.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma
jana, Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk Charles Tizeba alisema ushuru
unaotumika ni ule wa zamani badala ya mpya.
Tizeba alisema alishauriana na Waziri wa
Miundombinu wa Rwanda, Profesa Silas Rwakabamba na kukubaliana ushuru wa
zamani utumike wakati Serikali hizo zikiendelea na mashauriano. Alisema
Mawaziri wa Fedha wa Tanzania na Rwanda walitazamiwa kukutana ili
kuzungumzia suala hilo.
Dk Tizeba alisema juzi wafanyabiashara wa Tanzania
walipata usumbufu mkubwa baada ya kulazimika kulipa Dola 500 kuingiza
mizigo yao Rwanda badala ya Dola 152.
Hata hivyo, alikanusha madai kuwa Rwanda imepandisha ada hizo kutokana na mgogoro wa kisiasa baina ya nchi hizo.
No comments:
Post a Comment