Pages

Thursday, 24 October 2013

  Seif apongeza mkutano wa JK na vyama

MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, amempongeza Rais Jakaya Kikwete kwa kuzungumza na vyama vya siasa kuhusu Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba 2013, akisema ametumia njia sahihi kabisa.

Aidha, amesema itakuwa balaa kama Taifa kwenda katika Bunge la Katiba wakati bado kuna mvutano, na pia kama baada ya kupitishwa kwa Katiba, vyama vitaenda kwa wananchi kupiga kampeni ya kuzuia Katiba mpya.
Maalim Seif alisema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Unguja kuzungumzia miaka mitatu ya utendaji wa Serikali ya Awamu ya Saba ya Zanzibar, ambayo ni ya Umoja wa Kitaifa.
“Mimi nampongeza Rais Kikwete kwa kufanya mazungumzo na vyama vya siasa. Ametumia njia sahihi kabisa, nampongeza kwa asilimia mia moja,” alisema Maalim Seif na kuongeza:
“Itakuwa balaa kubwa sana kama tutakwenda katika Bunge la Katiba, kukiwa bado kuna mvutano, au kwamba baada ya Katiba kupita bungeni, vyama vitafanya kampeni ya kutaka Katiba isipite. “
Alisema njia ya mazungumzo aliyoitumia Rais Kikwete ndiyo mwafaka na pia maagizo yake kwamba vyama vyote ikiwamo CCM wakae na kuzungumza, ni sahihi.
“Matarajio yangu ni kwamba vikao vilivyofanyika na maazimio ya vikao hivyo, kati ya Rais na viongozi wa vyama vya siasa, yatazaa maafikiano mema, ili hatua zinazofuata katika suala zima la kuandika Katiba mpya ziendelee kwa amani na utulivu na matarajio ya wananchi walio wengi yafikiwe,” alisema Maalim Seif ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF).
Alisema Katiba lazima iwe shirikishi na ibebe maoni ya watu wengi, na kwamba wapo watu ambao wanataka kuuvuruga mchakato huo au kuifanya Katiba isiwe ya watu wengi, kwani suala hilo ni la makubaliano zaidi.
Aidha, alimpongeza Rais Kikwete kwa kuona umuhimu wa kuwashirikisha Watanzania wenyewe kuandika Katiba mpya, na kuongeza kuwa la msingi zaidi ni kuwa wananchi washirikishwe kikamilifu.
Mwanasiasa huyo mkongwe ambaye Oktoba 22, mwaka huu, alitimiza umri wa miaka 70, alisema ingawa alitoa maoni yake kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba wakati ikikusanya maoni hayo, chama chake hakina tatizo kwa sasa na Rasimu ya Katiba iliyotolewa maoni na mabaraza.

No comments: