Samaki wabovu waielemea Serikali
Msemaji wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Roida Andusamile amekiri
kuwa shirika hilo lilikutana na samaki hao kabla hawajaletwa nchini.
PICHA|MAKTABA
Kwa ufupi
Baadhi ya wakaguzi hawafanyi kazi yao ipasavyo, wamekuwa wakifika kwenye viwanda na kunyamazishwa na wamiliki.
Dar es Salaam. Afya za baadhi ya Watanzania
ambao ni walaji wa kitoweo aina ya samaki zimeendelea kuwa hatarini
kutokana na kuwapo kwa dalili kwamba Serikali imeshindwa kudhibiti uwepo
wa samaki wabovu katika soko la ndani, wanaoingizwa kutoka nje ya nchi.
Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi pamoja na
taasisi nyingine zinazohusika na udhibiti wa viwango na ubora wa samaki,
kwa nyakati tofauti wametoa taarifa ambazo hazionyeshi hatua
wanazochukua kudhibiti samaki hao, huku kukiwa na uthibitisho wa kuwapo
kwa samaki wabovu katika baadhi ya kampuni zinazofanya biashara hiyo.
Itakumbukwa gazeti hili katika toleo la Jumamosi,
Septemba 28, liliandika kuwapo kwa samaki hao sokoni, wakiuzwa kwa wingi
na kwa bei ya chini katika Soko Kuu la Kimataifa la Feri, Dar es
Salaam, lakini taarifa hiyo ilikanushwa na Katibu Mkuu wa Chama cha
Waingizaji wa Samaki Tanzania, Barnabas Mapunda kupitia baadhi ya
magazeti ya kila siku.
Mapunda huku akitetea vyombo vya Serikali
vinavyohusika na ukaguzi, alisema: “Napenda kuchukua fursa hii kukanusha
taarifa hiyo (Samaki hatari waingizwa nchini) na kuufahamisha umma wa
Watanzania si kweli kuwa samaki wanaoingizwa kutoka nje ya nchi
hawakidhi ubora na usalama kwa matumizi ya binadamu.”
Hata hivyo, siku chache baadaye Mamlaka ya Chakula
na Dawa Tanzania (TFDA), ilikamata kilo 7,500 za samaki aina ya vibua
walioharibika ambao waliingizwa nchini Julai mwaka huu na Kampuni ya
Sais Boutique kutoka China.
Kadhalika maelezo ya Mapunda yanatofautiana na
kile ambacho gazeti hili limekibaini ndani ya Kampuni ya Alpha Krust Ltd
ya Dar es Salaam ambayo taarifa zake za ndani zinathibitisha kuwapo kwa
samaki walioingizwa nchini ambao hawafai kwa matumizi ya binadamu.
Uchunguzi ulibaini kuwa samaki hao (Frozen Pacific
Mackerel W/R (Scomber Japonicus) waliingizwa nchini Agosti 29, 2013
kutoka Korea Kusini na Kampuni ya Wookyung Co. Ltd: 1851 Jangheung –don,
Nam-gu ya jijini Pohang na waliagizwa na Kampuni ya Alphakrust Ltd ya
Dar es Salaam.
Taarifa zaidi zinaonyesha kuwa mzigo huo ulibebwa
na Kampuni ya Mediterranean Shipping (T) Ltd. Taarifa zaidi zinaonyesha
kuwa samaki hao walizalishwa Juni 4, 2013 na tarehe ya mwisho kutumika
ilitakiwa kuwa Juni 3, 2014. Hata hivyo, chanzo cha kuaminika katika
kampuni hiyo kimebainisha kuwa tarehe hizo hazina uhalisia kwani samaki
hao walikuwa wameshaharibika na kuwa hizo ‘sticker’ huwa wanabandika tu,
lakini ukweli ni kwamba samaki wanakuja wakiwa wameshaharibika ndiyo
maana huwa wanauzwa kwa bei ya chini, kilibainisha chanzo hicho na
kuongeza:
“Kuna samaki walioharibika wa aina mbili, kwanza
kuna walioathiriwa na mionzi na kuna wale waliokaa muda mrefu. Hawa
waliopo ni waliokaa muda mrefu na ukitaka kuwajua hao samaki, watoe
katika barafu na kuwaloweka, utaona wanapasuka na ukitia kidole
wanabonyea. Athari yake kubwa ni ugonjwa wa saratani ya matumbo,”
kilieleza chanzo chetu.
Katika taarifa ya ukaguzi wa kitengo cha ubora cha
kampuni hiyo (Organoleptic Assessment) uliofanyika Septemba 12, 2013
(nakala tumeiona), sampuli nne za samaki zilithibitika kutofaa kabisa
kwa matumizi ya binadamu.
No comments:
Post a Comment