Pages

Thursday, 18 July 2013

SOKO JIPYA MWANJELWA UTATA



na Kelvin Lameck, Mbeya
MRADI mkubwa wa ujenzi wa Soko jipya la Mwanjelwa ulioanza baada ya soko lililokuwapo kuteketezwa kwa moto mwaka 2006, umekwama kumalizika kutokana na mkandarasi aliyepewa kazi hiyo kuishiwa fedha.

Uchunguzi wa umebaini kukwama kwa ujenzi wa soko hilo katika hatua za mwisho huku timu ya wataalamu kutoka Benki ya CRDB iliyotoa mkopo wa sh bilioni 13 wakihaha kufuatilia deni lao.

Benki ya CRDB iliikopesha Halmashauri ya Jiji la Mbeya fedha hizo ili kufanikisha ujenzi wa soko hilo na mkopo ulitakiwa utumike ndani ya miaka mitano na baada ya hapo jiji hilo lianze kurejesha mkopo huo na riba.

Kushindwa kukamilika kwa soko hilo ambalo ni kitega uchumi kikubwa katika halmashauri ya jiji hilo kumeibua hisia tofauti huku baadhi ya wafanyabiashara wakilalamikia uzembe uliofanywa na mkandarasi, Kampuni ya Tanzania Building Works Ltd (TBWL).

Mkurugenzi wa Tawi la CRDB Mbeya, Benson Mwakyusa, alisema ingawa si msemaji alikiri kupokea ugeni kutoka CRDB makao makuu na kwamba walikuwa na jukumu la kufuatilia masuala mengine ya kikazi na kukutana na mkopaji ambaye ni halmashauri ya jiji hilo, ili kuangalia njia nyingine ya kukamilisha ujenzi wa soko hilo.

Mhandisi mshauri wa ujenzi wa soko hilo, Dudley Mawalla, kutoka Kampuni ya MD Consultancy Limited alipohojiwa ili aeleze hali iliyosababisha ujenzi wa soko hilo usimame, naye aliruka na kudai kuwa si msemaji na anayetakiwa kusema ni mmiliki wa soko hilo ambao ni Jiji la Mbeya.

Mkurugenzi wa jiji hilo, Musa Zungiza, alikiri mkandarasi aliyepewa kazi ya ujenzi wa soko kushindwa kumalizia ujenzi licha ya kuomba aongezewe muda ambao nao ulimalizika na ndipo walipogundua kuwa aliishiwa fedha na ameshindwa pia kutimiza masharti waliyokubaliana.

“Sisi kama jiji hatumdai hadi pale alipofikia, kweli alituomba fedha, tulimuomba atupatie mpango mzima wa kazi na mtiririko wa fedha kutoka benki, tumefikia mahali tumekosana kwa kuwa hajatimiza masharti na tumezungumza na mhandisi mshauri ili tuone jinsi ya kumpata mkandarasi mwingine,” alisema Zungiza.

No comments:

Post a Comment